Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki imelaani vikali shambulio lililofanywa na wanajeshi wa Israeli dhidi ya wanadiplomasia, akiwemo balozi mdogo wa Uturuki, jiji la Jenin.
Katika taarifa yake siku ya Jumatano, Wizara hiyo imeliita shambulio hilo kama “tishio kubwa” kwa usalama wa diplomasia na linaakisi “jeuri na dharau ya Israeli kuhusu sheria za kimataifa na haki za binadamu.”
“Tunalaani vikali shambulio hilo dhidi ya wanadiplomasia akiwemo balozi mdogo wa Uturuki mjini Jerusalem,” ilisema taarifa hiyo.
Pia, ilisisitiza kuwa ilikuwa inahatarisha maisha ya wanadiplomasia.
Wito wa kufanyika uchunguzi
Wizara hiyo imetoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo, ikisisitiza kuwa wote watakaohusika, wawajibishwe.
Taarifa hiyo, pia imeitaka jumuiya ya kimataifa kuchukua msimamo thabiti kuhusiana na tukio hilo.
“Mashambulizi dhidi ya wanadiplomasia hayahatarishi usalama wao tu, bali pia usalama wa mahusiano ya nchi,” taarifa hiyo iliongeza.
Uturuki imezitaka taasisi za kimataifa kulaani tukio hilo na kuchukua hatua stahiki kutafuta suluhu ya jeuri na kiburi cha Israeli katika maeneo ya Palestina yanayokaliwa.
Hata hivyo, hakuna majibu yoyote kutoka kwa mamlaka za Israeli kuhusiana na tukio hilo.