Mshambuliaji Son Heung-min alikuwa miongoni mwa wachezaji wa Tottenham waliokosa medali za ushindi wakati wa hafla ya kusherehekea ushindi wa fainali ya Ligi ya Europa siku ya Jumatano.
Rais wa shirikisho la soka barani Ulaya UEFA Aleksander Čeferin alionekana kushangazwa wakati medali zilipoisha kabla wachezaji wote wa Tottenham kupata baada ya ushindi wao wa 1-0 dhidi ya Manchester United.
Baadaye UEFA ilisema kuwa sababu ni kutokana na Tottenham kupeleka watu wengi jukwaani kwa ajili ya kupokea medali wakati wa hafla hiyo.
Shirikisho hilo la soka barani Ulaya linasema vilabu viliarifiwa kuwa watu 30 pekee ndiyo wanaotakiwa kupokea medali. Linasema kuwa medali 20 zaidi zilitolewa kwa klabu hiyo baada ya hafla ili wapewe wachezaji na benchi la ufundi.
Son, ambaye alinyanyua taji hilo mbele ya wachezaji wenzake wakati wa sherehe, alikuwa miongoni mwa wachezaji wachache ambao hawakupata medali zao uwanjani. Hili lilikuwa taji kubwa kwa Tottenham tangu 2008.