Kurudisha ushirikiano wa kibiashara na Marekani itakuwa ndio kipaombele cha Rais Cyril Ramaphosa, ambae ameanza ziara yake nchini Marekani Jumatatu, ambapo atakutana na Rais Donald Trump, imesema ofisi ya Ramaphosa.
Ramaphosa aliwasili nchini humo Jumatatu jioni akiandamana na mawaziri wanne. Anatarajiwa kukutana na Trump katika ikulu ya White House Jumatano.
“Lengo la ziara ni kupanga upya na kudumisha uhusiano kati ya Afrika Kusini na Marekani,” imesema sehemu ya taarifa iliyotolewa na kurugenzi ya mawasiliano ya rais.
“Kufuatia hilo, ziara itajikita zaidi katika kuweka upya ushirikiano wa kibiashara na kiuchumi,” imeongeza kusema taarifa hiyo.
Uhusiano tata
Uhusiano kati ya Pretoria na Washington umekuwa tete tangu serikali ya Trump kuingia madarakani Januari.
Serikali ya Trump imekuwa ikilaumiwa kwa kufuata ushauri wa Elon Musk, mzaliwa wa Afrika Kusini ambae amekuwa akiongoza “Idara ya Serikali ya Ufanisi.”
Miongoni mwa mawaziri aliofuatana nao ni pamoja na waziri wa ushirikiano wa kimataifa, biashara na kilimo, pia mjumbe wake maalumu wa Marekani, Mcebisi Jonas.
Mshirika wa biashara
Marekani ni mshirika mkubwa wa pili wa biashara kwa Afrika Kusini, baada ya China.
Ushuru wa Trump uliotangazwa Aprili, na kuzuiwa kwa siku 90, umejumuisha ongezeko la ushuru wa asilimia 31 kwa bidhaa za Afrika Kusini, ambapo baadhi wa wamiliki wa viwanda wanasema inaweza kusababisha idadi kubwa ya watu kupoteza ajira.
Steenhuisen ambae ni kiongozi anayetetea sera za wafanyabiashara kutoka chama cha Democratic Alliance (DA) ambacho kimeungana na Ramaphosa kuunda serikali ya umoja wa kitaifa amesema wasiwasi mkubwa upo katika mustakbali wa mpango wa AGOA ambao unawezesha kufikiwa kwa soko la Marekani kwa bidhaa za Afrika.
Kuna hofu kwamba, serikali ya Trump itasitisha makubaliano hayo, ambayo yanatakiwa kupitiwa upya September.
“Makubaliano ya biashara kama vile ya AGOA yanachangia sana katika uchumi wetu,” amesema Steenhuisen katika taarifa yake.
“Kukosa manufaa haya itakuwa ni hasara kubwa kwa wakulima, wafanyakazi wa mashambani na uchumi kwa ujumla,” amesema.
Kiwango cha ukosefu wa ajira
Kiwango cha ajira nchini Afrika Kusini ni asilimia 32, hivyo suala la kuunda ajira mpya linabaki kuwa kipaombele kikubwa kwa serikali ya Ramaphosa.